Mike Tyson pichani hivi karibuni alihudhuria pambano la Juan Marquez na Diaz huko Mandalay Bay Las Vegas akiwa na mwanae wa kike ambapo alipokuwa huko alifanya mahojiano na radio ya ESPN.
Katika mahojiano hayo waliongelea juu ya maisha yake baada ya kustaafu mchezo wa masumbwi na hasa matumizi ya madawa ya kulevya ambapo alieleza hali ilikuwa mbaya sana na alishiriki kwenye filam ya Hangover ili aweze kupata fedha za madawa hayo na hakujua nini hasa kilimtokea mpaka akafikia hatua hiyo. Lakini hakutegemea filam hiyo ingekuwa na mafanikio makubwa iliyopata. Lakini hivi sasa Tyson ameacha matumizi ya madawa hayo. Nao watengenezaji wa filam hiyo wanafikiria kutoa Part II ambayo pia huenda Jammie Fox akawemo kwa mujibu wa Mike Tyson.
Katika mahojiano hayo pia alizungumzia kuhusu uzito wake ambao sasa amepunguza kutoka paundi 300 hadi 215 akidai kwamba unene ulimpa shida sana na alipoulizwa kitu gani kilimpa taabu alijibu kwa utani huku akicheka kwamba hasa baada ya kujisaidia shughuli ya usafi ilikuwa ni ngumu sana.
Aidha aliendelea kusema kuwa nguo anazovaa hivi sasa ni nguo alizokuwa nazo tangu miaka 15 hadi 20 iliyopita. Na pia alielezea amejifunza kupenda na kusamehe wakati wa Hija huko Mecca na kuhusu wanawake wazuri duniani alisifia kina dada wa Russia akidai aliona raia wa Russia weusi wazuri sana na hapo hapo aliongezea chachandu kwa kuwatania kina dada wa Afrika na Haiti kuwa wana mambo ya kishirikina mno.
Amehamia Las Vegas Nevada kwa sasa lakini amesema kuwa mkewe bado anaishi New York kwani hapendi kuishi Las Vegas na kuhusu muziki amesema hajui chochote kuhusu miziki ya Hip hop kwa sasa inaonekana amebadili maisha yake kwa kiasi fulani.




